WASHIKADAU katika sekta ya kutathmini ubora wa mbegu na pembejeo za kilimo wameendelea kushinikiza wakulima kununua bidhaa zao kutoka kwa maajenti walioidhinishwa na serikali. Pia wanaweza kutafuta ushauri kutoka kwa asasi maalum za serikali kama vile huduma ya ukaguzi wa afya ya mimea - Kenya Plant Health Inspectorate Service (KEPHIS). Wakulima pia wanahimizwa kutumia mfumo wa teknolojia ya ‘scanner’ katika hatua ya kupambana na wauzaji wa mbegu ghushi. Hili linajiri baada ya kubainika kuwa mbegu nyingi au pembejeo ambazo zimekuwa zikiwasilishwa sokoni hazikidhi mahitaji ya ubora. Matokeo yake hasi husababisha kiwango cha uzalishaji kudorora na upotevu wa mazao. Lawrence Kalawa, Meneja wa Ubora kutoka Bodi ya Kudhiti wadudu almaarufu Pest Control Products Board (PCPB), anasema pindi mkulima anaponunua pembejeo, anatakiwa kuhakikisha zimewekewa viashiria muhimu. Anasema, ingawa baadhi ya bidhaa zimepigwa marufuku humu nchini, bado zinasambazwa na kuwafikia wakulima kupitia mlango wa nyuma. Aidha matapeli wamekuwa wakiwapunja wakulima ambao hawana ujuzi wala utaalam wa kutofautisha pembejeo zinazofaa na zile ambazo ni ghushi. Anasema kwa mfano pembejeo ya Gladiator 4TC imebainika kuwa madukani licha ya matumizi yake kuwa hatari kwenye shughuli ya kuzalisha chakula. "Gladiator 4TC hutumika katika sekta ya ujenzi ili kukabiliana na mchwa au sisimizi ambao hushambulia mbao za nyumba," asema. Hii ikiashiria kwamba wakulima ambao wataendelea kutumia aina hii ya viuatilifu hawatapata matokeo mazuri katika hatua ya uzalishaji chakula. Pili, chakula kinachozalishwa kupitia aina hii ya pembejeo si salama kwa matumizi ya binadamu kwani huenda wakajiweka katika hatari ya kupata maradhi sugu yasiyoambukiza. Kalawa anasema kuwa uchunguzi wa maabara, uliofanywa na bodi ya PCPB unaonyesha matumizi ya ‘scanner’ kwa asili hutumika kuchanganua chembechembe tete. Vilevile umekuwa ukichukua sehemu muhimu katika hatua ya kuhakikisha kuwa vinavyopatikana ndani ya pembejeo ni salama. Hii ni kwa sababu baadhi ya tafiti zinaonyesha kuwa pembejeo huwa zimechanganywa na mafuta ya taa, maji au kemikali ambazo sio salama. Anasema mara nyingi biashara ghushi huendeshwa katika sehemu ambazo sio rahisi kwa maafisa wa PCPB kufika. Hata hivyo, anashauri kuwa mkulima anapogundua kuwa biashara hii ghushi inaendelea, anafaa kuripoti mara moja kwa maafisa wa usalama au idara husika ili mtuhumiwa achukuliwe hatua ya kisheria. Aidha anaweza kutumia teknolojia ya scanner kupitia njia ya simu ya mkononi ili kupata maelezo kuhusu bidhaa husika. Anasema mfumo huu wa kisasa utawasaidia wakulima kutambua usafi wa pembejeo za kilimo , ili wasitumie muda wao mwingi kuchambua nafaka kwa njia ya kubahatisha. “Scanner pia itawasaidia wakulima kupata taarifa muhimu kuhusu virutubisho vinavyopatikana kwenye pembejeo. Mchakato ambao utamsaidia kuweka utaratibu wa kufanyia mchanga wake uchambuzi kabla ya kuzamia hatua ya upanzi,” anaeleza. Anaongeza kuwa hatua hiyo ni pamoja na kuelewa siku ambayo bidhaa husika ilitengenezwa na pia muda wake wa kuharibika.Kupitia mfumo huu wa kutumia ‘scanner’ mkulima pia anaweza kutambua vitu vinavyopatikana kwenye pembejeo ambavyo vinaweza kusumbua mimea ama kuifaa.