Wakenya watalazimika kukaza mishipi zaidi huku ripoti ya hivi punde ya Shirika la Kitaifa la Takwimu Kenya (KNBS) ikionyesha bei za bidhaa muhimu zimepanda. Kulingana na ripoti iliyotolewa Ijumaa, Februari 27, bei za baadhi ya vyakula zimepanda. Kati ya Januari na Februari mwaka huu, bei ya sukuma wiki ilipanda kwa asilimia 2.4, huku ile ya kabeji na viazi kila moja ikiongezeka kwa asilimia 4.0. Sekta ya mikahawa na hoteli pia imeathirika na ongezeko hilo, ambapo bei ya chakula ilipanda kwa asilimia 0.8, na gharama za malazi katika nyumba za wageni zikiongezeka kwa asilimia 0.6. Huduma za elimu pia ziliathirika kidogo, ambapo karo ya kozi za cheti ilipanda kwa asilimia 0.1, zikichangia ongezeko la asilimia 3 kwa mwaka katika gharama ya elimu. Gharama za afya pia ziliendelea kupanda, huku huduma za hospitali na dawa kama za kuondoa minyoo na za shinikizo la damu zikigharimu zaidi. Vilevile, bidhaa za huduma za kibinafsi zilionyesha mabadiliko mchanganyiko huku bei ya karatasi shashi ikipanda kwa asilimia 1.4. Katika nguo, bei za shati za wanaume zilipanda kwa asilimia 4.1, huku bei ya makoti ya wanaume ikiongezeka kwa asilimia 2.7. Huduma za bima na kifedha pia zilipanda, ambapo bima za afya na magari zilipanda kwa asilimia 0.2 mwezi Februari, zikichangia ongezeko la asilimia 0.7 mwaka hadi mwaka. Huku bei za baadhi muhimu zikipanda, gharama ya uchukuzi ilishuka. Bei ya dizeli na petroli ilishuka kwa asilimia 2.3 kila moja, huku nauli za basi na matatu kati ya miji zikishuka kwa asilimia 1.4.