WATU 25 wamefariki dunia kufuatia mvua kubwa iliyonyesha usiku wa kuamkia Jumamosi, Machi 07, 2026 katika maeneo mbalimbali nchini hasa Nairobi na viunga vyake, huku mali nyingi ikiharibiwa na mamia ya wakazi kuathiriwa. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Idara ya Kitaifa ya Polisi, miili 13 zaidi ilipatikana kufikia Jumamosi alasiri, na kufikisha idadi ya waliopoteza maisha kutokana na mafuriko hayo kufikia 25. Msemaji wa polisi Muchiri Nyaga alisema mvua kubwa iliyosababisha mafuriko ilichangiwa pia na ukosefu wa mifumo bora ya mifereji ya maji, hali iliyosababisha maji kujaa kwa kasi katika maeneo ya makazi na barabara kuu. “Mvua kubwa imesababisha mafuriko makubwa yaliyopelekea vifo 23 kufikia sasa, uharibifu wa mali, kufungwa kwa baadhi ya barabara na watu kutoka makazi yao,” alisema Nyaga katika taarifa. Polisi walisema pia kuwa watu 29 waliokolewa kutoka maeneo mbalimbali na kwa sasa wanapokea msaada unaohitajika. Huduma za uokoaji ziliendelea usiku na mchana huku vikosi vya polisi vikishirikiana na mashirika mengine ya dharura kuwatafuta waliokwama kwenye maji au maeneo hatari. Kwa mujibu wa tathmini za awali za usalama na watoa huduma za dharura, maeneo yaliyoathiriwa zaidi ni pamoja na Mukuru, Kibra, Mathare, Huruma, South B, South C, Pipeline katika eneo la Embakasi, Roysambu, Kahawa West, Githurai pamoja na sehemu za Westlands. Aidha, sehemu kadhaa za barabara kuu pia ziliathiriwa na mafuriko hayo. Barabara zilizokumbwa na hali mbaya ni pamoja na Uhuru Highway, Mombasa, Thika Superhighway, Jogoo, Enterprise na Lang’ata, hali iliyosababisha msongamano mkubwa wa magari na baadhi ya njia kufungwa kwa muda. Polisi wamewahimiza wananchi kuwa waangalifu zaidi wanapotumia barabara na kuepuka maeneo yenye mafuriko makubwa. Wakati huo huo, Rais William Ruto ameagiza kupelekwa mara moja kwa wanajeshi wa Kenya (KDF) pamoja na kikosi cha pamoja cha mashirika ya dharura ili kuharakisha shughuli za uokoaji na msaada kwa waathiriwa. Katika taarifa yake ya kwanza rasmi kuhusu mafuriko hayo, Rais alisema mafuriko yanayoendelea katika Nairobi na maeneo mengine yamesababisha mateso makubwa kwa wananchi, ikiwa ni pamoja na kupoteza maisha, familia kuhama makazi yao na uharibifu wa mali na vyanzo vya riziki. Rais alisema operesheni hiyo ya dharura itaratibiwa na Wizara ya Usalama wa Ndani kwa ushirikiano na jeshi pamoja na mashirika mengine ya usimamizi wa maafa. “Nimeagiza kikosi cha pamoja kiundwe na kutumwa kuratibu juhudi za uokoaji, kusaidia jamii zilizoathiriwa na kuhakikisha watu walio katika hatari wanahamishwa haraka hadi maeneo salama,” alisema Rais. Serikali pia imetangaza kuwa italipia gharama za matibabu waathiriwa wa mafuriko wanaopokea matibabu katika hospitali za umma katika maeneo yaliyoathirika. Aidha, Rais ameagiza kutolewa mara moja kwa chakula cha msaada kutoka akiba ya taifa ili kusaidia familia zilizoathiriwa na mafuriko hayo. Katika juhudi za kupunguza mafuriko siku zijazo, serikali imesema mipango ya muda mrefu itawekwa ili kuboresha mifumo ya mabomba ya maji katika Nairobi na miji mingine mikubwa. Serikali ya kitaifa imekiri ukubwa wa maafa yaliyosababishwa na mvua kubwa inayoendelea kunyesha nchini, huku mafuriko yakiripotiwa katika kaunti kadhaa na kusababisha uharibifu mkubwa wa miundombinu. Waziri wa Utumishi wa Umma na Mipango Maalum, Geoffrey Ruku, alisema mafuriko yameripotiwa katika kaunti za Nairobi, Kiambu, Kajiado, Makueni, Nakuru, Migori, Murang’a, Bungoma, Kwale, Kirinyaga na Tharaka Nithi. Akizungumza wakati wa kikao cha mashirika mbalimbali katika Harambee House Jumamosi, Ruku alisema mafuriko hayo yameathiri maeneo ya mijini na vijijini kwa kiwango kikubwa. “Serikali imeanzisha mfumo wa kitaifa wa kukabiliana na dharura unaohusisha mashirika mbalimbali kusaidia katika shughuli za uokoaji na ukarabati wa miundombinu iliyoharibiwa,” alisema.