LA TAIFA LEO
CHAMA cha United Democratic Alliance (UDA) kimemulikwa baada ya ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Nancy Gathungu kubaini kuwa hakikukata wala kuwasilisha makato ya kisheria ya wafanyakazi wake kwa kipindi cha miaka mitatu, hali inayoweza kudhoofisha ukusanyaji wa mapato na mipango ya afya kwa wote inayopigiwa debe na kiongozi wa chama hicho, Rais William Ruto. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, UDA ililipa mishahara ya jumla ya Sh128.2 milioni katika miaka ya kifedha ya 2023/24 na 2024/25, lakini haikukata wala kuwasilisha ushuru wa PAYE, michango ya NSSF, Hazina ya Bima ya Afya ya Jamii (SHIF) wala ushuru wa nyumba nafuu. Wakaguzi walikadiria kuwa chama hicho kilipaswa kuwasilisha takriban Sh69.83 milioni kwa Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru Kenya (KRA), SHIF na Wizara ya Ardhi na Nyumba baada ya makato hayo. Ripoti hiyo inaonya kuwa kutotekelezwa kwa makato hayo kunanyima serikali mapato muhimu, huku pia kukiwaweka wafanyakazi katika hatari ya kukosa ulinzi wa kijamii unaotolewa kupitia mifumo hiyo ya kisheria. Aidha, hatua hiyo inaweka chama katika hatari ya kutozwa adhabu na riba kwa kutotekeleza wajibu wake wa kisheria. Zaidi ya hayo, ripoti hiyo ilibaini kuwa UDA pia haikukata ushuru wala ada za kujenga uwezo ilipolipa wasambazaji wake Sh219.35 milioni katika mwaka wa kifedha wa 2024/25, kinyume cha masharti ya Sheria ya Usimamizi wa Fedha za Umma ya mwaka 2012. Kwa mujibu wa sheria, wakandarasi wanapaswa kukata asilimia 0.03 ya malipo hayo kusaidia mafunzo ya wataalamu wa ununuzi katika taasisi za umma. Hata hivyo, afisa mmoja wa chama hicho ambaye hakutaka kutajwa jina alikanusha matokeo ya ripoti hiyo, akidai kuwa yalikuwa na makosa na hayakuonyesha hali ya sasa ya chama baada ya mabadiliko ya uongozi. Alisema UDA ina zaidi ya wafanyakazi wakujitolea 100,000 wanaopokea posho na hivyo hawastahili kukatwa PAYE, na kwamba chama kimefuata sheria kikamilifu. “Hatuna deni lolote. Tuna cheti cha utiifu kutoka KRA na hata SHIF. Mkaguzi alikosea,” alisema afisa huyo, akisisitiza kuwa changamoto zilizotajwa zilihusiana na usimamizi mbovu wa awali chini ya aliyekuwa Katibu Mkuu Cleophas Malala na mvutano wa kisiasa uliokuwapo wakati huo. Hata hivyo, Bw Malala alipuuza madai hayo, akisisitiza kuwa kwa kweli chama hicho hakilipi ushuru. “Tatizo linatokana na uongozi wa chama. Wakati fulani, vifaa vya kidijitali (tablets) vilivyoletwa kwa ajili ya uchaguzi wa mashinani viliingizwa nchini kinyume cha sheria bila kulipiwa ushuru wa forodha au kodi za uagizaji. Nilipoibua suala hilo katika kamati ya uongozi, nilifutwa kazi na kuambiwa ‘Serikali haiwezi lipa serikali’,” alisema Bw Malala katika majibu yake kwa Taifa Leo . Kiongozi wa chama cha Democratic Party, Justin Muturi alikosoa UDA, akisema haiwezekani chama kinachotawala kuhimiza wananchi kulipa ushuru huku chenyewe kikishindwa kutimiza wajibu huo. “Hauwezi kujenga uaminifu kwa kuhimiza utekelezaji wa sheria huku ukihepa kufanya hivyo. Hauwezi kuwataka wananchi kujitolea wakati wewe unakwepa,” alisema. Kinyume na ahadi za Rais Ruto za kuhakikisha kila Mkenya analipa ushuru, ripoti hiyo inaonyesha kuwa UDA huenda ikachangia pengo la mapato lililoshuhudiwa na KRA katika mwaka wa kifedha wa 2024/25, ambapo shirika hilo lilikosa kufikia lengo lake la Sh2.305 trilioni kwa pengo la Sh48 bilioni. UDA ilipokea Sh481.4 milioni kutoka Hazina ya Vyama vya Kisiasa, pamoja na Sh154.9 milioni kutoka kwa wanachama na michango mingine. Hata hivyo, matumizi makubwa ya kiutawala na kisiasa yaliacha chama na nakisi ya Sh39 milioni. Ripoti hiyo pia iligusia ukiukaji wa masharti ya ajira jumuishi, ikibainisha kuwa chama hakikuwa na mfanyakazi yeyote mwenye ulemavu, kinyume cha Katiba inayotaka angalau asilimia tano ya nafasi za kazi katika taasisi za umma zitengewe watu wenye ulemavu. Vilevile, chama hakikutenga fedha kwa mipango ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kama inavyotakiwa kisheria. Ripoti ya Nancy Gathungu inaibua maswali makubwa kuhusu uwajibikaji wa vyama vya siasa, hasa vile vinavyoongoza serikali, na inaweka shinikizo jipya kwa UDA kujieleza na kurekebisha kasoro zilizogunduliwa. Maelezo ya ziada na : Benson Matheka
Go to News Site