Mwananchi
Tokana na ufyatu, leo naja kifalsafa kama mwanafalsafa nguli ambaye hajawahi kutokea isipokuwa mimi. Sipigi pembeni wala kuzungusha. Leo nipo na ‘mabeberu’ yanayowabeberu mabebera hadi wanalalamika kama vichanga mbali na kubumburuka tokana na kubumburushwa na mabeberu. Jamaa hawa wanatisha usipime. Mabeberu, hayawani au mafyatu ni viumbe dhalili, hatari, na hovyo. Huchukiana, kushukiana, kuchukuliana, kuibiana, kuogopana, kuogopeshana, na kusingiziana. Huchukua vya wenzao wakichukia vyao kuchukuliwa. Kwao, kila fyatu ni mbuzi jike. Kwanza, kwanini mabeberu yaliitwa mabeberu na siyo madume? Kwa waliowahi kufuga au kuchunga mbuzi, wanajua namna mabeberu yanavyowabumburusha majike lau kuijaza dunia na kutupatia nyama. Kiasili, mabeberu siyo viumbe wabaya. Maana, wasingekuwapo, hata nyama choma isingekuwapo. Pamoja na nia na uzuri wao, mabeberu huwa yanafanya makeke na kusababisha mikikimikiki na mshike mshike hadi wapate wanachotafuta. Kila beberu akitaka mambo, utamsikia akibembeleza mbuzi jike bee bee beeebeee hadi mswahili anasema hili linabembeleza jike tu. Jamani, huu siyo ustaarabu uliokiuka hasa kwa dunia ya mafyatu wabakaji hadi wanabaka hata kaya? Kwa lugha rahisi, beberu hubembeleza jike tofauti na fahari ambalo hurukia tu na kupata mchezo. Tuachane na mabeberu mbuzi. Tuje kwa mafyatu. Kimsingi, kwa mafyatu, mabeberu si wamakonde bali watasha. Tena ni wakwasi usipime. Ukiwapendeza wanakupiga njuluku hadi unaona kuwa kubomu na kukopa ndiyo utaratibu wa maisha hasa kwa zile kaya uchwara zinazokalia mali na kuendekeza kubomu bomu na kukopa kopa. Mabeberu hupenda sana kaya hizi. Uzuri ni kwamba Fyatuland haimo kwenye kundi hili uchwara linalojivua nguo hadharani wakati mali linazo ila linazikalia. Japo tunawaponda mabeberu, ni kama tunajisahau kuwa huwa, wao, tofauti na mabeberu ya mbuzi, huwa tunajipeleka kwao wenyewe. Hivyo, sioni kama ni ufyatu badala ya uzwazwa kulalamika pale wanapoacha kutubembeleza. Hata hivyo, kila fyatu hata wadudu wanajua. Badala ya wao watubembeleze kama mabeberu wafanyavyo kwa majike, siye huwa tunawabembeleza pale tunapotaka kuwatoa njuluku. Hapa, jina beberu hubadilika na kuwa mfadhili. Waswahili wana msemo kuwa mfadhili mbuzi, fyatu ana maudhi. Alichanacho fyatu, sawa na mabeberu, ni ukosefu na wizi wa fadhila. Ukimpa fyatu njuluku, unaitwa mfadhili, mdau, mshirika na majina mengine matamu. Hepu muulize kazitumiaje. We, utakoma. Utaitwa beberu kana kwamba una akili kidogo kama mbuzi. Huu nao upuuzi tena wa wazi ufanywao na mafyatu chizi wazijue twajua. Mafyatu wana mambo. Ukiwa mfadhili ukawanyima njuluku wanakunanga hasa unapostukia rongorongo zao juu ya namna walivyotumia njuluku ulizowafadhii au kuwakopesha. Ukiwastukia, jiandae. Ghafla watageuka na kujifanya hamnazo kama siyo kujitoa ufahamu waanze kukuponda pale walipokuingiza chaka kuwa wanakupenda. Ama kweli, wasohaya wana mji wao. Si unajua sizitaki hizi mbichi? Japo wanajitia kulalamika lau waonewe huruma, mafyatu bumburushwa wana tabia kama ya mafahari aka madume ya ng’ombe. Tokana na ufahari wao, tena uchwara na kupenda ufahari wakati ni mafakiri wa kunuka, hujifaharisha hadi kujisahau na kuwadharau, kuwathumu, hata kuwatukana mabeberu wawapao fahari feki waipendayo na kuifuja. Utakuta mifyatu haichapi kazi. Badala yake inachapa majungu na starehe.Mingine inakwapua njuluku za mafyatu kwa mikono miguu na midomo utadhani itaishi milele. Mingine kazi yake ni kujikombokomba kama chawa na inzi. Halafu inataka eti nayo iheshimike au kufanikiwa kama kaya zilizoukata wakati kaya yao ikiendelea kuwa ombaomba na kopakopa! Loo! Mingine inapiga njuluku tena ndefu ya mafyatu wenzao na kuishia ima kuifuja au kuificha ughaibuni. Mingine, inapoteza njuluku kuzurura kama yule habithi wa Kireno Vasco da Gama au yule Mbayuwayu wa zama zile aka Njaa Kaya. Halafu yakiambwe mfanyayo siyo yanagomba, kuzoza, kulalama, na kuwatukana wafadhili kuwa ni mabeberu. Kama ubeberu ni rahisi, ujaribuni muone. Kama mabeberu ni wabaya, mbona mnajipeleka wenyewe? Kama mabeberu ni mabaya, mbona mnapenda nyama choma? Kwani waliofilisi kaya ni hao mabeberu au mabu na mafisi na mafisadi? Huwa nashangaa mafyatu wazima kuogopa mabeberu wakati mbuzi majike, pamoja na uhayawani wao, hawawaogopi. Wakipewa maji, wanatoa wana mbuzi na mafyatu tunakula nyama. Sasa hapa, ubaya wa mabeberu uko wapi? Tukiwa wakweli, nani si beberu tena hata wengine majike? Nazoza hivi kwa sababu mabeberu, licha ya kuwa mafahari, hupenda ufahari. Huwa ni shapu yanapotaka vitu. Yanaweza kupata kwa kudandia au kubembeleza beebeeebeeebebe. Kinachofanya nipende mabeberu, kwanza, huwa hayana chawa. Pili, huwa si manafiki. Yakitaka kitu, kila kit uni mambo hadharani. Hamjayaona yanavyowakimbiza na kuwabeberu majike siyo? Ukiachia mbali ubeberu kuonekana jambo baya hasa wale wanaoitwa mabeberu wanapostuka, hata wale wanaoukandia, ima wanao, kwa kujua au kutojua, au wanautamani na kuuonea gere. Nani asiyependa ubeberu ili awabeberu wenzake? Nenda kawaulize wahanga wa kweli wa ubeberu kama wale Gen Ziro wa kaya ya kufikirika jirani na Fyatuland. Du! Kumbe hii bangi kali!
Go to News Site