LA TAIFA LEO
KAULI ya Waziri wa Kawi na Petroli Opiyo Wandayi, kwamba Kenya ina akiba ya kutosha ya mafuta imeendelea kuzua utata, huku hali halisi ikionyesha vituo vingi vya mafuta kote nchini vimeanza kukosa bidhaa hiyo muhimu. Bw Wandayi alijaribu kutuliza hofu ya wananchi jana kwa kusema kuwa hakuna uhaba wa mafuta kwa sasa, na kwamba serikali imeweka mikakati madhubuti ya kukabiliana na hali yoyote ya dharura. Alisema Kenya pia inatafuta mbinu mbadala iwapo kutatokea usumbufu katika mpango wa Serikali kwa Serikali unaohusisha kampuni za Saudi Aramco, Abu Dhabi National Oil Company na Emirates National Oil Company. “Hakuna mgogoro kwa sasa. Tuna akiba ya kutosha ya bidhaa zote za petroli. Tunawahimiza Wakenya kuepuka kununua mafuta kwa hofu,” alisema Wandayi, akiongeza kuwa serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu hali ya vita Mashariki ya Kati. Hata hivyo, uchunguzi unaonyesha hali tofauti kabisa. Vituo kadhaa vya mafuta vinavyomilikiwa na Vivo Energy, ambayo inadhibiti karibu asilimia 20 ya soko la Kenya, vimeripotiwa kukosa petroli na dizeli. Baadhi ya vituo katika kaunti za Kilifi na Mombasa vimefungwa kabisa baada ya kuishiwa na mafuta, huku kampuni nyingine zikichagua kukaa kimya kuhusu hali hiyo. Jijini Nairobi, wateja walikosa mafuta katika vituo kadhaa vya Vivo, hasa katika maeneo ya Karen, Ong’ata Rongai, Kiserian na kituo kilichoko karibu na Kipande House. Hali hii imeongeza wasiwasi miongoni mwa wananchi kuhusu uwezekano wa uhaba mkubwa katika siku zijazo. Wataalamu wa sekta ya mafuta wanaonya kuwa hali inaweza kuwa mbaya zaidi katika wiki za kwanza za Aprili, hasa kutokana na kukosekana kwa meli zinazobeba mafuta katika bahari kwa sasa. Inatarajiwa kuwa meli ya kwanza kufika katika Bandari ya Mombasa itawasili mapema mwezi ujao, jambo linaloacha pengo kubwa katika usambazaji. “Kwa sasa hakuna meli yoyote baharini. Hii ina maana kuwa ikiwa hatutapata suluhu ya haraka, nchi inaweza kukumbwa na mgogoro mkubwa wa mafuta ndani ya wiki chache zijazo,” alisema mmoja wa wadau wa sekta hiyo. Hali hii tayari imesababisha ununuzi wa hofu ambapo madereva wengi wanajaza magari yao mafuta kikamilifu kwa hofu ya uhaba. Baadhi ya wauzaji wameanza kuuza kwa vipimo au kuwapa kipaumbele wateja wanaolipa pesa taslimu badala ya wale wanaonunua kwa mkopo. Changamoto hii inachochewa zaidi na hali ya kisiasa na kiusalama katika eneo la Mashariki ya Kati, hasa baada ya mashambulizi ya Iran dhidi ya miundombinu ya mafuta, jambo ambalo limeathiri uzalishaji na usafirishaji wa mafuta kupitia Mlango wa Hormuz. Njia hii ni muhimu kwa usambazaji wa mafuta duniani, na usumbufu wowote huathiri soko la kimataifa. Athari za mgogoro huu tayari zimeanza kushuhudiwa kimataifa. Nchi kama Slovenia zimeanza kuweka viwango vya ununuzi wa mafuta, huku Sri Lanka na Bangladesh pia zikigawa mafuta kwa kiwango maalum ili kudhibiti matumizi. Kwa upande wa Kenya, serikali sasa inakabiliwa na changamoto mbili kuu; kuhakikisha kuna mafuta ya kutosha sokoni na wakati huo huo kudhibiti kupanda kwa bei. Ili kukabiliana na hali hiyo, serikali imeweka ruzuku ya Sh6.53 kwa kila lita ya dizeli na Sh0.14 kwa petroli, huku mafuta ya taa yakipata ruzuku ya Sh6.66 kwa lita. Hata hivyo, wadau wa sekta ya mafuta wanaonya kuwa huenda serikali italazimika kuongeza ruzuku hiyo zaidi kutokana na kupanda kwa bei ya mafuta ghafi duniani, ambayo ilivuka dola 100 kwa pipa mwezi uliopita baada ya kuzuka kwa vita.
Go to News Site